Kambi maalum ya madaktari bingwa chini ya mpango wa Mama Samia imewasili rasmi Mkoani Iringa kwa lengo la kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi ambapo Kambi hiyo itatoa huduma katika Halmashauri tano za Mkoa huo, ikiwemo Iringa DC, Kilolo, Mufindi, Iringa Manispaa na Mafinga na Mpango huo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi, hasa walioko vijijini na maeneo ya pembezoni.
Akizungumza wakati wa mapokezi ya Madaktari hao Juni,02,2025,Kaimu mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Credinus Mgimba amesema kuwa ujio wa Madaktari hao Bingwa utasaidia wananchi kupata matibabu ya kibingwa bila gharama kubwa na usumbufu wa kusafiri kutoka Iringa kwenda kupata matibabu mkoa mwingine.
Jumla ya madaktari bingwa 36 wamepokelewa rasmi kwa ajili ya kutekeleza huduma hizo, wakijumuisha wataalamu wa fani mbalimbali za tiba. Kwa mujibu wa ratiba ya kambi hiyo, madaktari hao watazunguka katika halmashauri husika kwa siku kadhaa ili kuwahudumia wagonjwa wenye uhitaji wa huduma za kibingwa ambazo kwa kawaida hupatikana katika hospitali za juu au rufaa pekee.
Ikumbukwe kuwa utekelezaji wa mpango huu, kwa awamu ya kwanza zaidi ya wananchi 2,500 walinufaika na huduma mbalimbali za kibingwa, wakiwemo wagonjwa 274 waliopatiwa huduma za upasuaji na wengine 238 waliopata rufaa kwa matibabu ya juu.
Zaidi ya wagonjwa 3,000 hadi 4,000 wanatarajiwa kuhudumiwa katika kipindi chote cha kambi hiyo. Wananchi wengi tayari wamejitokeza kwa wingi katika vituo vilivyopangwa wakionesha hamasa kubwa na matumaini kutokana na ujio wa huduma hizo muhimu.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, 4 Barabara ya Pawaga
Anuani ya Posta: P.O.Box 858, 51108 Gangilonga, Iringa, Tanzania
Simu: +255 262 702 715
Mobile:
Barua pepe: ras@iringa.go.tz
Hakimiliki ©2025, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Iringa.